Saturday 22 March 2014

Padri akuta tunguli Kaburini kwa NGWEA! Zimevishwa sanda zikiwa na majina ya watu ....hofu yatanda

Ooo…Nooo! Wakati hati ya kifo cha aliyekuwa rapa bora Bongo, marehemu Albert Keneth Mangweha ‘Ngwea’, ikiendelea kushikiliwa nchini Afrika Kusini alikokutwa na umauti mwaka jana, kwenye kaburi lake kumekutwa tunguli zilizozungushiwa sanda,Risasi Jumamosi linakupa mchapo kamili.
Tunguli hizo zilikutwa Ijumaa ya wiki iliyopita na Padri wa Kanisa Katoliki Parokia ya Mtakatifu Monica, Kihonda mkoani Morogoro, Octavian Msimbe ambapo ziliibua hofu miongoni mwa waumini wa kanisa hilo lililopo katika eneo hilo la makaburi.

PADRI AKEMEA

Awali, ilielezwa kuwa siku hiyo padri huyo alioteshwa ndoto usiku juu ya uwepo wa vitu vya ajabu katika makaburi hayo ndipo akakemea kabla ya kwenda kuvishuhudia asubuhi yake (Ijumaa iliyopita) huku paparazi wetu akinyetishiwa na kuwahi eneo la tukio.

PAPARAZI USO KWA USO NA PADRI

Paparazi wetu alipofika eneo la tukio alikutana uso kwa uso na kiongozi huyo wa kiroho akiwa amesimama kwenye kaburi hilo la Ngwea.

Paparazi wetu alipomfikia Padri huyo alimuuliza kulikoni ndipo alipomsimulia kisa kizima. “Jana (Alhamisi ya wiki iliyopita) nilioteshwa juu ya kuwepo kwa vitu vibaya kwenye makaburi haya ya waumini wetu ambayo yapo nje ya kanisa letu. “Nilishtuka sana na kuona mambo ya ajabu, nikaamua kushusha maombi ya kukemea ambapo nilioteshwa kuwepo kwa vitu kwenye makaburi yetu ambayo yako jirani kabisa na sehemu ninayo lala,” alisema Padri Msimbe na kuongeza: “Leo kulipokucha ndipo nikafika kwenye makaburi haya na kuanza kukagua yote likiwemo la Mangweha (Ngwea) nikayakuta yakiwa na tunguli zilizovishwa sanda ambazo pia zina majina ya waumini wangu wa moja ya vigango vya parokia hii.”

AKATAA KUTAJA MAJINA
Alipoombwa kutaja majina ya waumini hao alisema: “Sitaweza kutaja majina yao wala ya kigango yaliyoandikwa kwani wanajijua wenyewe na mbaya zaidi hata waumini wataona katika ibada Jumapili hii (Jumapili iliyopita), nitaonesha madhabahuni,” alisema padri huyo ambaye tangu alipofika kwenye kanisani hilo limekuwa na maendeleo makubwa.

Kama alivyoahidi, ilipofika Jumapili iliyopita, padri huyo akiwa madhabahuni alisitisha mahubiri kisha akatoa tunguli hizo na sanda na kuwaonesha waumini. Aliwatangazia waumini hao kuwa vitu hivyo alivikuta kwenye kaburi hilo ambapo alisema kuwa sanda hizo zilikuwa zimeandikwa majina ya baadhi ya wafuasi wa kanisa hilo ndipo kukaibuka hofu hivyo ikabidi maombi ya nguvu yafanyike.
Pamoja na maombi ya nguvu lakini walioona majina ya baadhi waumini wenzao kwenye sanda hizo, walianza kushikwa na mshangao huku wakitazamana usoni. Paparazi wetu alifikia kwenye ibada hiyo na kujionea jinsi waumini walivyotaharuki kutokana na vitendo hivyo ambavyo vilitokea katika makaburi hayo.“Mimi hata sielewi maana kwa jinsi ninavyoona, itakuwa kuna watu wasio na hofu ya Mungu wanaendekeza mambo ya kishirikina, sasa wanaandika haya majina lakini najua kwa kuwa tumeyabaini, kwa nguvu za Mungu, watashindwa,” alisema muumini mmoja ambaye hakupenda jina lake lichorwe gazetini.
Paparazi wetu alizidi kutafuta data zaidi juu ya sakata hilo ambapo mwishoni alijiridhisha kuwa tunguli hizo zilipokewa na waumini, zikahifadhiwa katika ofisi ya Padri Msimbe. Mbali na tunguli hizo zilizokutwa katika kaburi la Ngwea, mwandishi wetu alijionea kiroba cha tunguli hizo zilizozungushiwa  sanda katika ofisi ya padri huyo zilizohifadhiwa chini ya meza. Minong’ono zaidi ilizidi kuibuka kuwa huenda watu walioweka tunguli hizo kuwa wameweka katika kaburi la Ngwea ili waweze kung’ara kimuziki kama alivyokuwa marehemu. “Watu wanadanganyana, wamesababisha waumini wengi kuingiwa na hofu juu ya nini hatma yao. Wanaamini mtu anaweza kufariki dunia na mwingine akatembelea nyota yake, tunapaswa kuishi katika matakwa ya kumuamini Mungu siku zote,” alisema muumini mwingine wa kanisa hilo ambaye ni kiongozi kanisani hapo.
Kwa hisani ya GPL

0 maoni: