Monday 4 November 2013

AFYA YA UZAZI : Kisukari kwa mama mjamzito

Madhara ya kisukari  wakati wa ujauzito yamegawanyika  katika sehemu kuu tatu yaani kwa mtoto ambaye bado hajazaliwa, kwa mama mwenyewe na kwa mtoto aliyezaliwa
Mtoto aliyeko tumboni
Kiwango cha kuharibika kwa mimba kiko juu zaidi kwa wajawazito wenye kisukari kuliko wale ambao hawana.
Katika hatua za mwisho za mimba kisukari huleta madhara katika mfumo wa utendaji kazi wa kondo la nyuma kiasi kwamba mtoto aliye tumboni hushindwa kupata hewa ya kutoshana hasa kama pia yapo matatizo mengine kama kondo la nyuma kuachia , shinikizo la damu  na uzazi  kuchukua muda mrefu.
Kasoro za kimaumbile pia hutokea kwenye kundi hili. Watoto wa kina mama wenye kisukari huzaliwa na uzito mkubwa kuliko kawaida na hivyo kusababisha uzazi kuwa wa taabu kutokana na uwiano mbaya kati ya kichwa cha mtoto na ukubwa wa nyonga ya mama na  kuzaa kwa njia ya upasuaji.
Madhara kwa mjamzito
Wakati wa ujauzito, kisukari mara nyingi huwa  kinayumba na kuwa vigumu kukudhibiti na hasa kipindi cha wiki ya 12 na wakati wa kukaribia mwisho wa kipindi cha mimba.
Kinamama wengi huongeza kiwango chao cha mahitaji ya insulini kwa kiasi kikubwa japo idadi ndogo huendelea na kiwango kile kile na hata hupunguza.
Mahitaji ya juu ya insulini yanaweza yakatokea wakati wowote ule wakati wa kujifungua na hivyo ni muhimu kupima sukari mara tu baada ya kujifungua kwani mahitaji ya insulini hurudi katika hali ya kawaida ya kabla ya ujauzito  baada ya siku chache za kujifungua.
Madhara makubwa kwa mama mjamzito hutokea kwenye macho, figo na mishipa ya damu. Haya huweza kuthibitiwa kwa kiasi kikubwa kama kisukari kitafuatiliwa na kusimamiwa kwa karibu.
Uwezekano wa kupata kifaa cha mimba huwa ni mara mbili zaidi kuliko kwa wajawzito ambao hawna kisukari.
Kibaya zaidi, wajawazito hawa huwa kwenye hatari zaidi kama wameongezeka uzito kupita kiasi kwani hili nalo huongeza kiwango cha insulini  inayotakiwa.
Kwa hisani ya Mwananchi

0 maoni: