Friday 26 April 2013

LEMA anatafuta umaarufu wa kisiasa kwa faida ya nani?!

TAHADHALI IKIKUKWAZA ACHANA NAYO.... 


Wakuu habari ya Sikukuu?,natumaini hamjambo wote,kwa wale wagonjwa poleni mungu atawasaidia mtapona. Kwa muda mrefu nimekuwa nafuatilia siasa za Mbunge wa Arusha Mjini Godbless Lema,na kujiuliza maswali mengi mengine nimekuwa sipati majibu hata kidogo.
Tafadhalini naomba tujadili hili kwa uungwana mkubwa ili tusije tukaondoa maana halisi ya maudhui yangu,Tangu kuingia kwake madarakani Arusha hakujatulia,kila siku ni migogoro na vurugu ambazo mwisho wake ni lazima mtu apotee maisha!. Kwa wale wenye kumbukumbu sahihi mtakubaliana na mimi kwamba katika uongozi wake watu si chini ya wanne wamekwishapoteza maisha kutokana na vurugu,sitaki kuingia kwa undani juu ya hili lakini kwa wale wenye kumbukumbu nadhani mnalitambua. 

Ni huyu huyu Lema ambaye amejikuta mara kadhaa akitolewa Bungeni kama si kukwazana na viongozi kadhaa ndani ya Bunge kutokana na maneno yake kadha wa kadha haijalishi iwe kweli ama si kweli,lakini yametokea!. Mara nyingi nimekuwa pia nikufuatilia kauli zake kwenye mikutano mbalimbali ya hadhara,ukisikiliza kwa makini uangundua kwamba Lema ni Mtata,ni mtu ambaye anaonekana kukata tamaa ya maisha na sasa kujaribu kutumia njia za mkato ikiwemo jazba kutafuta ufumbuzi. 

Nimemsikia mara nyingi sana akithibitisha kwamba hapendi kuonewa na pale anapobaini kwamba anataka ama ameonewa basi ni lazima asimame kidete kujitetea ama kutetea haki yake,hili ni jambo ni sahihi na namuunga mkono,lakini tunatofautiana katika kuidai hii haki,yeye anatumia nguvu kubwa zaidi. Kuna viongozi wengi sana ambao ukiwatizama wamefanya mambo makubwa na mazito katika kuhakikisha kwamba wanajitetea ama kuwatetea na wengine ama wale wanaowaongoza,lakini wamekuwa wakitumia hoja ambazo mwisho wa siku zinaleta mana halisi. 

Kwa mfano yupo JOHN MNYIKA, ZITTO KABWE, DK.SLAA, HALIMA MDEE,na wengineo wengi wa leo,jana na juzi,lakini hatuwahi kusikia vurugu kwenye maeneo yao wala watu kuuawa,nilitegemea kwamba Baada ya Lema kurudi Bungeni na kwa sababu amekiangusha chama kikubwa kama CCM angetulia na kujaribu kuwaonyesha watanzania kwamba yeye ni mtu wa namna gani katika nchi hii,lakini matarajio yangu yamekuwa tofauti. 

Ndiyo mana nashawishika kuamini kwamba pengine Lema anatafuta umaarufu kutokana na hivi vituko vyake vya kila siku!,lakini ni vituko ambavyo vinaanza sasa kumfanya adharaulike katika jamii,kwa sababu watu wanaanza kuzoea kwamba LEMA ni wa vurugu. Ombi langu kama Lema atatoka na kurejea tena mitaani,kuna haja ya viongozi wa CHADEMA kukutana nae na kujaribu kuzungumza nae,mbona wenzake wanakua na hoja na zinapenya na kupokelewa vizuri na jamii?!,kwa nini aisijifunze kwa wenzake. 

Mwisho hakuna mtu anayependa kuonewa hapa Duniani,hata mtoto mdogo ambaye bado ananyonya akiona mama yake anamsumbua sana kwenye titi huwa anapiga ngumi ama kuficha na kupiga mateke kuashiria kwamba hapendezwi na yanayojitokeza.Narudia Lema akitoka salama Polisi na kurejea mitaani aachane na hizi vurugu akae na wananchi wake wafanya shughuli za maendeleo,naamini wameshaelewa madhumuni yake.

Mdau - Wabheja Sana

0 maoni: